Hayo yamedokezwa na Hujjatul Islam Ali Moqanni, Mkuu wa Taasisi ya Mashindano ya Qur'ani katika Shirika la Wakfu la Iran ambalo huandaa mashindano ya kimataifa ya Qur'ani nchni. Ameongeza kuwa wasomi 35 wa Qur'ani Tukufu kutoka Iran pia watakuwa katika jopo la majaji wa vitengo mbali mbali vya mashindano hayo. Hujjatul Islam Moqanni amesema mashindano ya mwaka huu yatakuwa na kitengo cha kawaida cha wanaume na kisha kutakuwa na vitengo maalumu vya wanawake, watu wenye ulemavu wa macho, wanafunzi wa vyuo vya kidini na wanafunzi wa shule.
Halikadhalika amesema kitengo cha wenye ulemavu wa macho kitakuwa na mashindano ya kuhifadhi Qur'ani pekee huku vitengo vikingine vilivyosalia vikiwa na mashindano ya kuhifadhi Qur'ani na kusoma kwa tajwidi.
Mashindano ya kimataifa ya Qur'ani mwaka huu nchini Iran yatakuwa na washiriki 600 kutoka nchi 81 ambao wameshashiriki katika awamu ya kwanza ya mchujo kabla ya kuja Iran.
Fainali za Mashindano ya 36 ya Kimataifa ya Qur'ani Tukufu zimepangwa kuanza mjini Tehran kuanzia Aprili 10 katika Ukumbi wa Sala wa Imam Khomeini mjini Tehran.
Shirika la Wakfu la Iran huandaa mashindano ya kimatiafa ya kusoma na kuhifadhi Qur'ani ya Iran kila mwaka ambapo huwa na washiriki kutoka kila kona ya dunia.
Mwaka jana kulikuwa na washiriki 370 wa kigeni waliohudhuria mashindano ya kimataifa ya Qur'ani.