IQNA

Hamas yapendekeza uongozi mpya kwa ajili ya umoja wa Palestina

18:05 - June 30, 2020
Habari ID: 3472914
TEHRAN (IQNA) –Kiongozi wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Kupigania Ukombozi wa Palestina (Hamas) amependekeza mfumo mpya wa uongozi wenye kujumuisha wote ili kupatikane umoja wa kitaifa Palestina.

Kiongozi wa Hamas Ismail Haniya amesema: "Sisi kama Hamas tumeanzisha mkakati wa kuhakikisha kuna umoja wa Palestina."

Akizungumza katika mazungumzo yaliyoandaliwa na Wakfu wa Yedi Hilal, Haniya amesisitiza kuwa kuna udharura wa kuwa na umoja wa taifa wakati huu ambapo Wapalestina wanakabiliana na njama ya Israel ya kupora ardhi zaidi za Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.

Wakati huo huo, Haniya amesema utawala wa Kizayuni wa wa Israel unafuatilia malengo matatu makuu katika mpango wake wa kutaka kutwaa ardhi ya Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.

Katika mahojiano na shirika la habari la NetTV la Uturuki na kufafanua kuwa, lengo la kwanza la utawala huo pandikizi wa la kupora maeneo zaidi ya Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na Quds ni kuwafukuza Wapalestina katika ardhi zao kwa mujibu wa Sheria ya Utaifa ya 2018 ya utawala huo.

Hania amesema lengo la pili la Tel Aviv katika mpango huo ambao umekosolewa vikali na jamii ya kimataifa ni kupora asilimia 30 ya Ukingo wa Magharibi, na kutekeleza njama za kufanya mashariki na magharibi mwa Quds tukufu kuwa mji mkuu usiotenganishika wa utawala huo haramu.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Hamas, lengo la tatu la utawala bandia wa Israel ni kuzuia uundwaji wa taifa huru la Palestina, na kwa njia hiyo uwe umefanikiwa katika azma yake ya kusambaratisha kadhia ya Palestina na kuwafurusha Wapalestina zaidi katika ardhi zao.

Utawala haramu wa Israel umepanga kutekeleza mpango wa kutwaa asilimia 30 ya eneo la Palestina la Ukingo wa Magharibi na kuliunganisha na ardhi nyingine zilizoghusubiwa za Palestina ifikapo tarehe Mosi mwezi Julai mwaka huu wa 2020. 

Mpango wa utawala haramu wa Israel wa kutwaa asilimia 30 ya eneo la Palestina la Ukingo wa Magharibi na kuliunganisha na ardhi nyingine zilizoghusubiwa za Palestina ni miongoni mwa vipengee muhimu vya mpango wa kibaguzi wa “Muamala wa Karne”. Benjamin Netanyahu, kiongozi wa chama cha Likud na Benny Gantz kiongozi wa chama cha Blu na Nyeupe, walifikia makubaliano ya kutwaa asilimia 30 ya eneo la Palestina la Ukingo wa Magharibi na kuliunganisha na ardhi nyingine zilizoghusubiwa za Palestina. Mpango huo umepingwa vikali na Wapalestina na jamii ya kimataifa.

3471838

captcha