Aliyekuwa Askofu Charles Okwany, wa kanisa ambalo lilikuwa likijulikana kama God's Call Church of East Africa alisilimu baada ya kufanya utafiti wa kina kuhusu Uislamu. Kanisa hilo lilikuwa katika kijiji cha Nyalgosi eneo la Rangwe Kaunti ya Homa Bay magharibi mwa Kenya.
Okwany alisilimu pamoja na idadi kubwa ya wafuasi wake na kuligeuza kanisa lake kuwa msikiti. Askofu huyo wa zamani aliukubali Uislamu maishani na kutamka shahada mbili mnamo Septemba 26 mwaka 2017 na hapo alibadilisha jina lake na kuwa Ismail Okwany.
Hatimaye Februari 14 mwaka 2019, msikiti uliojengwa katika ardhi ya zamani ya kanisa ulifunguliwa rasmi katika sherehe ambayo mgeni wake rasmi alikuwa ni imamu wa Msikiti wa Jamia wa Nairobi Sheikh Muhammad Swahilu. Taarifa zinasema katika ufunguzi wa msikiti huo unaojulikana kama Nyalgosi Mosque, watu watano akiwemo mwanamke walisilimu.
Ismail Okwany anasema moja ya sababu zake za kusilimu ni vazi la Hijabu katika Uislamu. Anasema akiwa mhuburi alikuwa anakerwa sana na wanawake waliokuwa wakiingia kanisani wakati wa ibada wakiwa wamevalia sketi fupi huku wakikaidi ushauri wake wa kuvaa mavazi ya heshima. Anasema wanawake wanaovaa mavazi kama hayo yasiyofaa kanisani huwa wanawachochea wahubiri kutenda dhambi.
Anaongeza kuwa, "Wakati nilipokuwa askofu, nilisafiri hadi Nairobi, Mombasa na Malindi nchini Kenya na pia katika nchi jirani ya Tanzania kuhubiri. Nilitumia fursa hiyo kujifunza kuhusu maisha na tabia za Waislamu na Wakristo katika maeneo niliyotembea na nikafikia natija kuwa, Uislamu ndio mfumo bora zaidi wa maisha."
Ufunguzi wa Msikiti wa Nyalgosi
Ismail Okwany alipotangaza kusilimu
Waliosilimu katika kijiji cha Nyalgosi wakiswali nje mwaka 2017 kabla ya msikiti kujengwa