Ayatullah Ahmad Khatami ameashiria vitisho vya rais wa Marekani dhidi ya Iran na kusema, Marekani ni nchi yenye kuvunja ahadi na kwamba muqawama ndio njia pekee ya kusimama kidete na kukabiliana na madola ya kiistikbari.
Khatibu wa Sala ya Ijumaa ameongeza kuwa ni kosa kuwategemea Wamagharibi hasa Wamarekani kwani hivi sasa Marekani inazungumza kuhusu vikwazo vipya dhidi ya Iran.
Ayatullah Khatami amelaani jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel katika eneo la Mashariki ya Kati na dhidi ya Wapalestina na kusisitiza kuwa, utawala huo ni ghasibu na kama alivyosema Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, ifikapo miaka 25 ijayo, utawala wa Israel hautakuwepo.
Khatibu wa Sala ya Ijumaa Tehran ameashiria kuhusu oparesheni za kigaidi huko Brussels, Ubelgiji na kusema, "Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inalaani oparesheni za kigaidi kote duniani." Aidha amekosoa mtazamo wa kindumakuwili wa nchi za Magharibi kuhusu ugaidi katika nchi za Syria na Iraq na kusema, mtazamo huo umesababisha maafa kwani magaidi sasa wamewageukia Wamagharibi.
Ayatullah Khatami ameashiria hatua ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kutangaza mwaka mpya wa 1395 Hijria Shamsia kuwa mwaka wa 'Uchumi wa Kimuqawama, Hatua na Vitendo' na kusema, uchumi wa kimuqawama au kimapambano unapaswa kuwa kwa maslahi ya Iran.